Maalim Seif apinga mauaji ya Padri asema si ya kigaidi
Baada ya mauaji ya Padre Evarist Mushi, akizungumza na wandishi wa habari,Nchimbi alielezea kusikitishwa na mauaji hayo akisema kuwa ni ya kigaidi na yana lengo la kuingiza nchi katika machafuko. Amesema kuwa tukio hilo si tukio la ujambazi bali tukio la kigaidi kwani limelenga zaidi katika kuwashambulia viongozi kidini.
Padre Evaristus Mushi aliuawa Februari 17, mwaka huu kwa kupigwa risasi na watu wasiojulikana waliokuwa katika pikipiki aina ya Vespa wakati akienda kuongoza misa katika Kanisa la Mtakatifu Theresia la Beit el Rass.
“Watu hawa wameamua kuyatumia matukio ya kuuawa na kujeruhiwa kwa viongozi wa kidini ili kuvunja umoja wa Wazanzibari, lakini nasema hakuna ugaidi Zanzibar,” alisema Maalim Seif juzi usiku alipohutubia kwenye hafla ya Maulid ya kuzaliwa kwa Mtume Muhammad (S.A.W) mjini Kiuyu, Wilaya ya Wete, Kaskazini Pemba.
Hata hivyo, Maalim Seif alisema inasikitisha kuona wakati Rais Jakaya Kikwete katoa maelekezo uchunguzi wa kina ufanyike na Kamishna wa Polisi Zanzibar ameshaweka wazi kuwa uchunguzi unaendelea, baadhi ya viongozi na vyombo vya habari vinachochea chuki za kidini na kusema kuwa Zanzibar kuna ugaidi.
Aliwataka wananchi wote wa Zanzibar kwa wakati huu kuwa watulivu na wasitawaliwe na jazba na wala wasichokozane, pia wasikubali kuchokozeka.
Akizungumzia matokeo ya mtihani wa kidato cha nne yaliyotolewa hivi karibuni, Makamu wa wa Kwanza wa Rais alisema ni matokeo mabaya na ya kuliza, kwa sababu hayaonyeshi mustakabali mwema kwa watoto wetu na nchi yetu hapo baadaye.
Alisema ni wakati mwafaka Serikali, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, walimu na jamii nzima kujiuliza nini sababu ya matokeo hayo mabaya, na kujiuliza pia nchi inaelekea wapi?
Maalim Seif alisema sasa si wakati tena wa kutupiana lawama, lazima pande zote zikae zijadili wapi pamekosewa, ili ufumbuzi uweze kupatikana na hali kama hiyo isitokee tena siku nyingine.