Kufa kumeumbiwa kiumbe chochote kilicho hai. 
Kama kilizaliwa basi siku moja kitakufa. Lini kitakufa hakuna ajuaye 
labda yule aliyepanga mauaji ya kiumbe hicho na wakati mwingine hata 
yeye muuaji anafikia hatua asifanikiwe katika azma yake hiyo. Kwa sisi 
wenye imani za dini tunaamini kwamba Mungu alitupa ruhusa ya kutoa uhai 
wa mimea na wanyama ili kujifanyia chakula. Wapo wanaoondoa baadhi ya 
wanyama kwamba nao hawaruhusiwi kwa imani zao.
                
              
Pia wapo wale wanaoondoa wanyama wote na kubaki na
 ruhusa ya kutoa uhai wa mimea tu. Katika wote hao sijasikia wanaosema 
kwamba imani yao imewapa ruhusa ya kutoa roho za watu wengine. Hivyo 
kila mwenye kuamini kwa imani yake anaamini kwamba mwenye haki na roho 
ya binadamu ni yeye aliyemuumba yaani Mungu anayemwamini. Pamoja na 
ukweli huo ambao bahati nzuri wengi wetu tunauamini bado wapo watu ambao
 wao wanafikiria wamepata ruhusa ya kutoa roho za watu wengine.
                
              
Tuwaache wale wenye kupewa kazi ya kunyonga au 
wanajeshi wanaokwenda vitani ambao hao mjadala wao ni tofauti na hawa 
ninaowazungumzia. Mimi nazungumzia wale ambao kazi walizopewa ni 
kuzifikisha roho za watu salama kule ziendako hapa duniani yaani 
madereva wa mabasi ambayo yanasafirisha abiria. Watu hawa naona 
wamesahau kwamba wana jukumu hilo. Ajali zinazotokana na magari ya 
abiria zimekuwa nyingi mno na kwa asilimia kubwa utaambiwa chanzo ni 
uzembe wa dereva. Hatuwezi kuendelea kuufumbia macho uzembe huu! Ni 
lazima tufanye kitu kwa madereva hawa waliojiajiri kutoa roho za watu.
                
              
Dereva aliyekamilika yaani ni mtu mzima, hajalewa,
 hana ugonjwa wa akili, kwa jumla anajitambua sawasawa na bila shaka 
anajua kwamba roho ya binadamu ikitoka haina mbadala. Pia anajua kwamba 
alichokibeba ndani ya gari hilo kina thamani kuliko vitu vyote ambavyo 
Mungu ameviumba.
                
              
Haiwezekani kabisa kwa dereva kama huyo kuamini 
kwamba fedha anazozisaka ni muhimu kuliko hao binadamu. Kwanza hata kama
 anapenda fedha kuliko watu atapata wapi watu wa kumpatia hiyo fedha 
kama yeye kazi yake ni kuwapunguza kila siku? Kwa sababu hiyo mimi 
naamini kwamba hawa madereva wanaoendesha magari ya abiria ambao kila 
kukicha tunawasikia kwa uzembe huu na ule uliosababisha maafa ya 
kupoteza uhai wa watu, au kuwapatia vilema vya kudumu ni watu wenye 
hitilafu fulani katika ubinadamu wao kama siyo akili zao.
                
              
Maana wewe unajua umebeba roho za watu ambazo 
hazina mbadala lakini kichwani kwako unachofikiria ni fedha iliyoko 
katika kituo kinachofuata kiasi kwamba hujali namna unavyoyapita magari 
yaliyo mbele yako. Akili yako inakuwa imevurugukiwa kiasi kwamba hatari 
ya kugongana uso kwa uso na gari iliyopo upande huo unaopita huifikirii 
bali unachokiona ni fedha zilizopo kituo hicho unachokikimbilia.
                
              
Nasema huu ni uwazimu kwa sababu pamoja kwamba 
tunasema binadamu anatakiwa kuthubutu ili apate anachohitaji lakini 
kuthubutu huko huwa kunafanyika kwa mahesabu; yaani asilimia gani 
umeweka ya kufanikiwa katika mkakati wako? Ukifanikiwa utapata nini?
                
              
Ukikosa utapoteza nini? Sasa katika hali ya 
kawaida kabisa inaonesha kwamba uwezekano wa kufanikiwa kuyapita magari 
yaliyo mbele yako bila kupata ajali ni mdogo. Kwa uwezekano huo mdogo 
bado ni kwamba ukishindwa utapoteza maisha ya watu. Kweli unacheza 
kamari ya uwezekano mdogo wa kufanikiwa na kupata vinauli dhidi ya 
uwezekano mkubwa wa kushindwa na kupoteza maisha ya watu? Kama huko siko
 kukosa hekima ni nini?
                
              
Mimi nafikiri wakati umefika sasa wa kupandisha 
viwango vya watu wanaotaka leseni za udereva wa kubeba abiria. Kama vile
 ilivyo kwa kazi nyingine nyeti kama usalama wa taifa basi na udereva 
nao ungechukuliwa hivyo hivyo.
                
              
Watu wachunguzwe hata katika maisha yao ya 
kawaida, namna wanavyoyapokea mambo mbalimbali yanayohusu jamii, namna 
wanavyofanya uamuzi pale inapobidi wafanye uamuzi kati ya fedha au vitu 
na watu na mengine. Vigezo hivyo wapewe wamiliki wa vyombo ili 
kuhakikisha kwamba wanaajiri watu wanaojitambua katika kazi hizo.
                
              
Bila kufanya hivyo tutaendelea kuwa na madereva 
hawa wasiojali, wasiojitambua, wasiokuwa na ubinadamu na ambao wameamua 
kujiajiri kwenye kazi ya kunyonga watu.
                
              
Baada ya hapo sheria pia zirekebishwe kuhakikisha 
kwamba anayefanya uzembe barabarani na kupoteza maisha ya watu basi 
asikabidhiwe tena roho nyingine maana yake asiruhusiwe tena kuwa dereva 
wa magari ya abiria.
Huyo mmiliki wa gari naye asijinasue kwenye mkono wa sheria 
mpaka hapo atakapothibitisha kwamba yeye alitimiza sehemu yake kwa 
kuajiri dereva mwenye viwango. Pia anampatia dereva wake huyo mwenye 
viwango muda wa kupumzika kwa kuhakikisha kwamba haruhusu dereva huo 
mwenye viwango kuendesha gari toka saa kumi asubuhi mpaka saa sita usiku
 bila mapumziko.
                
              
Kama dereva hana viwango au kama mwajiri hajafanya
 mpango wa dereva kupumzika kwa kumuwekea dereva mwingine kwa gari 
linalohudumia zaidi ya muda wa kawaida wa kufanya kazi basi sheria 
imgeukie mwajiri, naye asiruhusiwe kuhudumia umma katika biashara ya 
kubeba abiria.