SKENDO nzito inalitafuna Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ikitawala madai kwamba kuna wabunge wawili wanawake, wamejazwa mimba na waheshimiwa wenzao wanaume.
Awali, ulitawala uvumi kuwa mmoja wa wabunge wa upinzani (viti maalum), akitokea Kanda ya Kaskazini, amepewa ujauzito na mheshimiwa mwingine ambaye ni kiongozi anayeshika nafasi za juu kwenye moja ya vyama vikuu vya upinzani nchini (wote majina yao tunayahifadhi kwa sasa).
Kashfa hiyo ya mtunga sheria huyo kupewa mimba na mheshimiwa mwenzake ambaye ni mume wa mtu, ilipata mbeleko na kuifanya ivume zaidi, baada ya Mbunge wa Mtera (CCM), Livingstone Lusinde, kulipuka bungeni: “Humuhumu ndani kuna wabunge wanawake wenye mimba zisizotarajiwa.”
Lusinde, alitamka hayo Aprili, mwaka huu, wakati akichangia hotuba ya bajeti, Ofisi ya Waziri Mkuu, kipindi ambacho bunge lilikuwa limechafuka kutokana na wabunge kurushiana ‘mipasho’ wao kwa wao.
Kauli ya Lusinde, pamoja na kupokelewa tofauti na wabunge wengi wanawake, wakidai mheshimiwa mwenzao amewadhalilisha, upande mwingine, katika ‘vikao vya kwenye korido’, matukio ya vicheko na kugonga mikono yalitawala na kunena kwa msisitizo “message delivered”, yaani ujumbe umefika.
Katika kufanyia kazi kila kinachozungumzwa, mwandishi wetu alizungumza na baadhi ya wabunge ambapo Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika, alisema: Unajua madai ya mimba yanawahusu wanawake, kwa hiyo waulizwe wenyewe.
“Kama umenitafuta mimi kwa kigezo kwamba ni mbunge kijana, basi waulize wabunge vijana wanawake,” alisema Mnyika.
Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila, alikiri kufahamu kuwepo kwa tuhuma kwamba wapo wabunge wamepeana mimba lakini hawezi kuwa na uhakika kwa sababu uhusiano wa kimapenzi ni jambo la faragha.
“Hayo madai yapo, yanazungumzwa. Wapo wanaotajwa kuwa na uhusiano wa kimapenzi, hayo ni mambo ya faragha. Sijui pengine walioanzisha haya madai wana vipimo vyao,” alisema Kafulila.
Mbunge wa Viti Maalum (CCM) Mkoa wa Morogoro, Sara Msafiri, alisema kuwa haiwezekani wabunge kupata mimba zisizotarajiwa kwa sababu ni watu wazima.
“Wabunge tunapata mafunzo ya uzazi, kwa hiyo kama ni mimba basi mtu anakuwa amepanga kuipata. Hakuna kitu kama hicho. Hata hilo la kutoa mimba halipo kabisa, sijawahi kusikia mtu amefanya hivyo bungeni,” alisema Sara.
Mbunge mwingine wa Viti Maalum (Chadema), Chiku Abwao, alisema: “Hakuna mbunge anayepata mimba isiyotarajiwa, kwanza nilimshangaa mbunge kutamka mambo kama hayo, alistahili kuwaambia watoto, lengo lake lilikuwa kudhalilisha wanawake.”
Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Munde Tambwe, alisema: “Ile kauli ya Lusinde kwamba kuna wabunge wanapata mimba zisizotarajiwa, nadhani kuna mtu alikuwa anamlenga, kwa hiyo mimi siwezi kulizungumzia.”










































