Saturday, June 22, 2013

NCHI IMEVAMIWA


Stori:Mwandishi wetu

Taifa linapepesuka, linayumbishwa na adui asiyeonekana, anayesababisha kizaazaa kisha yeye kukaa pembeni akiwaacha Watanzania wao kwa wao wakinyoosheana vidole kutuhumiana kuhusika.

IGP Saidi Mwema
Adui huyo ameivamia Tanzania na ndiye inafaa awe mtuhumiwa nambari moja wa bomu lililolipuliwa Soweto, Arusha, katika mkutano wa hadhara wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) wakati wa ufungaji wa kampeni za uchaguzi mdogo wa udiwani, Jumamosi ya wiki iliyopita.

Jinsi nchi…
Stori:Mwandishi wetu
Taifa linapepesuka, linayumbishwa na adui asiyeonekana, anayesababisha kizaazaa kisha yeye kukaa pembeni akiwaacha Watanzania wao kwa wao wakinyoosheana vidole kutuhumiana kuhusika.

IGP Saidi Mwema
Adui huyo ameivamia Tanzania na ndiye inafaa awe mtuhumiwa nambari moja wa bomu lililolipuliwa Soweto, Arusha, katika mkutano wa hadhara wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) wakati wa ufungaji wa kampeni za uchaguzi mdogo wa udiwani, Jumamosi ya wiki iliyopita.
Jinsi nchi inavyopepesuka kwa sasa, ni ishara ya mafanikio ya adui huyo ambaye lengo la uvamizi wake na harakati zake za kutibua amani ya nchi kuona Watanzania wao kwa wao wanashikana mashati, badala ya kuzingatia masuala muhimu yanayohitaji mshikamano wa kitaifa.
Namna Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chadema, vinavyotuhumiana kuhusika na ulipuaji wa bomu hilo ambalo imeshaelezwa kusababisha vifo vya watu wanne, ni ushindi kwa adui huyo mwenye shabaha ya kutenda tukio kiuchochezi na kuzigeuza fikra za watu kutuhumu wasiohusika.
“Tuache kufikiria haya mambo kisiasa, tuyatafakari katika sura yenye hoja mahususi, utaona kwamba siyo CCM wala Chadema wanaohusika na ulipuaji wa bomu Arusha,” alisema Job Ngarano, mkazi wa Arusha, aliyejitambulisha kuwa msomi wa shahada ya kwanza ya Diplomasia na Uhusiano wa Kimataifa.

NANI KALIPUA BOMU?
Ripoti ya uchunguzi wa gazeti hili, iliyokusanya taarifa za eneo la tukio na mambo mengine ya pembeni kuhusiana na bomu la Arusha, imebaini kuwa siyo Chadema wala CCM, mwenye uhakika na tuhuma dhidi ya mwenzake.
Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, alishatoa kauli yenye kudai kuwa anao mkanda wa video unaoonesha namna tukio lilivyotendeka na akasisitiza kuwa mlipuaji ni askari polisi aliyekuwa amevalia sare za kikosi cha kutuliza ghasia (FFU).
Upande mwingine, Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alirusha kombora kwamba Chadema ndiyo wahusika wa bomu hilo.
Tuhuma za Nape, zinaendana na dhana kuwa Chadema walijilipua wenyewe kwa lengo la kutafuta huruma ya wapiga kura ili wakichague chenyewe katika uchaguzi mdogo wa udiwani, uliofanyika Juni 16, mwaka huu.
Uchunguzi unapingana na dhana hiyo kwa hoja kwamba Chadema kilikuwa na nafasi kubwa ya kuibuka mshindi katika uchaguzi huo bila hata kusaka huruma ya wapiga kura, kutokana na jinsi kilivyokuwa kinakubalika.
 Macho yanayoona mbali aliyonayo Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia, January Makamba, ndiyo yaliyomuongoza pale alipowataka wanasiasa kukaa kimya na kuacha mamlaka zinazohusika kufanya kazi yake.
“Natoa rambirambi zangu na kulaani. Naamini katika mambo haya ni vyema wanasiasa tukafunga midomo yetu hadi ukweli ujulikane,” January, aliandika ujumbe huo kuhusiana na tukio la Arusha, kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter.
Wakati January akiwataka watu kutulia na kuacha kusemasema, Noel Kyaro ambaye ni mwongozaji wa watalii (tour guider) Arusha, alisema kuwa kama Chadema na CCM, watakaa pamoja na kuacha kutuhumiana, wanaweza kumpata kwa urahisi mhusika wa mabomu.
“Kuna changamoto nzito hapa, inabidi pia tuangalie uhusiano wa nchi yetu na mataifa mengine. Tanzania inaonewa wivu sana kutokana na uimara wake wa vivutio vya utalii,” alisema Kyaro na kuongeza:
“Hivi karibuni Rais wa Rwanda, Paul Kagame, alitoa kauli chafu sana dhidi ya Rais Jakaya Kikwete. Sasa haishindikani Rwanda kufanya huo ugaidi kwa sababu wameonesha waziwazi kupitia kwa rais wao kuwa hawatupendi.”
Rwanda inapotajwa, moja kwa moja kikundi cha waasi cha chini DRC cha M23, kinaingizwa katika skendo hiyo kwa sababu haijapita muda mrefu tangu nacho kiutangazie ulimwengu kuwa kitapambana na Tanzania.
Mei 5, mwaka huu (Jumapili), saa 4:30 asubuhi, bomu lilirushwa kwenye Kanisa Katoliki la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi, Parokia ya Olasiti, Arusha na kusababisha vifo vya watu watatu na majeruhi zaidi ya 40.
Siku moja kabla, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, alitoa tamko la serikali kuwa Tanzania lazima ipeleke majeshi DRC kupigania amani na haitishwi na vitisho vya waasi wa M23.
Kauli ya Membe, ilifuatia waraka wa M23 ambao waliutuma nchini, wakieleza kuwa ni ujumbe kutoka kwa Mungu, wakiionya Tanzania kutopeleka majeshi DRC, vinginevyo itakiona cha moto.
Baada ya kauli hiyo ya Membe, M23 walihamishia mashambulizi yao kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter, wakiitishia Tanzania.
Baadhi ya ‘twiti’ za M23, siku moja kabla ya bomu la kanisani Arusha, mojawapo ilisema: “Membe usiwadanganye watu, mnakuja DRC kuweka petroli kwenye moto, hamji kutafuta amani.”
Twiti nyingine inasomeka: “Hatutishwi na scout (askari chipukizi), Tanzania leteni majeshi yenu halafu mtaona.”
Hatari kubwa zaidi ni kwamba M23, walitishia kuingia nchini na kufanya mashambulizi, wakitamba wana uwezo mkubwa sana wa kufanya hivyo.
Kutokana na hatari hiyo, Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe, ‘alitwiti’, akionya kwamba M23 walikuwa ‘wanatwiti’ wakiwa Dar es Salaam, hivyo ni dhahiri kuwa kundi hilo lilikuwa limeshaingia nchini.
Kauli hiyo ya Zitto, ilikuwa inaweka wazi namna taifa letu lilivyo hatarini, kwani maadui wanaweza kuingia nchini na kupanga mashambulizi dhidi yetu bila sisi wenyewe kujua.
“Kabla ya kurushiana makombora na kutuhumiana bila ushahidi ni bora tukaangalia uhusiano wa nchi yetu na mataifa mengine. Nchi majirani zetu hazitupendi, wanatuonea wivu, hawashindwi kupanga njama za kutuchonganisha sisi kwa sisi,” alisema Matilda Urio wa Kijenge Chini, Arusha na kuongeza:
“Hatutamjua adui, hatutapata ufumbuzi wa haya matatizo mpaka tutakapoacha kutuhumiana sisi kwa sisi. Chadema waache kuwalaumu CCM kuwa wanahusika, vilevile CCM wasiituhumu Chadema. Tuhuma hizo zinapoteza uelekeo wa kumjua adui.”
Mtumiaji wa Twitter mwenye akaunti yenye jina @iAlen, aliandika ujumbe wake kwa Lugha ya Kiingereza; This Chadema CCM blame game isn’t going to help anyone. People have lost their lives here folks (Huu mchezo wa kulaumiana CCM na Chadema hautamsaidia yeyote. Watu wamepoteza maisha).

KWA NINI
NI WATU WA NJE?
Kwa mujibu wa watu waliozungumza na gazeti hili ambao wanalitazama tukio la Arusha kwa jicho la mbali zaidi ni kwamba sura ya nchi kiutalii ndiyo inayosababisha jiji hilo likumbwe na misukosuko ya milipuko ya mabomu.
“Unalengwa utalii wetu, majirani wanataka Tanzania ionekane ina machafuko ili watalii wawe wanaenda kwenye nchi zao,” alisema Rachel Komba ambaye ni Meneja Uhusiano wa Taasisi Isiyo ya Kiserikali ya OTSG.
Rachel alisema: “Jinsi tunavyogombana ni sawa na mgonjwa wa kifafa halafu arogwe ugonjwa wa malaria ya kichwa, akianguka, kila mtu atajua kifafa ndicho kimemfanya aanguke.
“Tanzania kuna udini, kuna mvutano mkubwa wa kisiasa kati ya CCM na Chadema. Bomu likitupwa kanisani, haraka sana Wakristo wanawatuhumu Waislamu, vilevile bomu likitupwa kwenye mkutano wa Chadema, wafuasi wa Chadema watawatuhumu CCM.
“Tuliona jinsi bomu la kanisani Arusha lilivyoleta sintofahamu, vilevile hili la mkutano wa Chadema, linavyowagombanisha CCM na Chadema. Kuna adui wa nje anayewachonganisha Watanzania.
“Anafanya makusudi kwa kutumia udhaifu wetu. Anajua tuna udini, anapiga upande mmoja halafu Waislamu na Wakristo wanakamatana, amepiga mkutano wa Chadema, tunaona hali ilivyo.”
Rachel aliongeza: “Inakuwa vigumu kuwajua hawa maadui kwa sababu wanatupiga kwa kutuchonganisha. Kama wangelipua reli au bandari, moja kwa moja tungejua ni wavamizi kutoka nje. Tatizo wanapiga makanisa, misikiti na mikutano ya vyama vya siasa ndiyo maana inatuchukua wepesi kutuhumiana sisi kwa sisi.”
Elibariki Munishi wa Unga Limited, Arusha, alikumbusha tukio la bomu ambalo alipigwa Katibu wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata), Mkoa wa Arusha, Sheikh Abdulkarim Jonjo, akiwa nyumbani kwake na kumjeruhi vibaya.
“Inawezekana kabisa, watu waliomrushia bomu Sheikh Abdulkarim ndiyo haohao waliolishambulia kanisa na ni haohao waliorusha kwenye mkutano wa Chadema. Inabidi tuwe makini sana.
“Tukidanganyika, tunaweza kupigana sisi kwa sisi. Hakuna Muislamu Mtanzania anayeweza kumdhuru Mkristo, vilevile Mkristo hawezi kumdhuru Muislamu kutokana na asili yetu na tunavyojijua,” Elibariki.

LENGO LA NINI?
John Sebless wa Ngarenaro, alisema kuwa lengo la adui ni kuvuruga sura ya utalii wa nchi, hivyo kuyafaidisha mataifa ya kigeni.
“Haya machafuko malengo ya wachafuaji ni kuifanya nchi yetu ionekane siyo salama kwa kupokea watalii. Halafu jiulize kwa nini Arusha ambayo ndiyo mji ambao unaoongoza kwa utalii nchini?
“Tunatakiwa kuacha kulumbana na kusimamia utaifa wetu. Adui kutoka nje anatugawa, tuache kuzingatia mambo ya msingi na matokeo yake tubaki tunalumbana wenyewe. CCM hakiwezi kulipua bomu Chadema kwa sababu viongozi wake wana akili na wanajua kufanya hivyo, wao watakuwa watuhumiwa nambari moja.
“Vilevile haiingii akilini Chadema kujilipua wenyewe. Tuache kulumbana, Wakristo kwa Waislamu, Chadema, CCM na vyama vingine vyote, tunatakiwa tutambue kwamba tumevamiwa kisha tuanze kupambana na adui huyo wa nje anayetaka kuvuruga sifa njema ya nchi yetu kiutalii,” alisema Sebless.
Hata Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, mapema wiki hii, alithubutu kulinyooshea kidole jeshi la polisi, akalitaka kuacha kutumia mabomu kutuliza machafuko, akafafanua kwamba kufanya hivyo kunazidi kuuweka utalii wa nchi katika hali mbaya.

KUTOKA KWA MHARIRI
Tunapaswa kulinda amani yetu ambayo inavutia watalii na wawekezaji wengi kuja nchini. Tuamke sasa na kupambana na adui anayetaka kuivuruga nchi yetu. Bila umoja na mshikamano hatutashinda. Tusikubali kuchochewa kupigana sisi kwa sisi. MHARIRI.

0 comments: