Sunday, July 14, 2013

RAY C AFUTUKA

Stori: Mwandishi  Wetu
Mwanamuziki staa wa Bongo Fleva, Rehema Chalamila ‘Ray C’ ambaye amepotea katika anga la muziki kwa kipindi kirefu kutokana na matatizo ya matumizi ya madawa ya kulevya, amejitokeza akiwa amefutuka.
Hivi karibuni, Ray C ameibuka na kuanza kutundika picha na vipande vya video zake katika kurasa zake kwenye mitandao ya kijamii, ikiwa ni sehemu ya kujiweka karibu na mashabiki wake.
Kufuatia ishu hiyo, kumeibuka mshtuko mkubwa kwa baadhi ya watu kutokana na picha hizo kumuonesha ‘bidada’ akiwa amenenepeana ghafla tofauti na alivyozoeleka.

UNENE UNATOKANA NA DOZI?
Baadhi ya mashabiki wake katika mtandao wa Instagram walidai kuwa inawezekana unene huo unatokana na dozi ya kuacha ‘unga’.
Hata hivyo, wengine walimshukuru Mungu kwa kuwa sasa afya ya mwanadada huyo inaonekana kurudi katika hali yake ya kawaida tofauti na miezi kadhaa aliporipotiwa na gazeti hili akiwa amezimika kutokana na matumizi ya unga.

AFUTUKA
Katika picha hizo, Ray C anaonekana kufutuka usoni, kifuani na mapajani ambapo awali kabla ya matatizo hakuwa hivyo.
Wengi walimshukuru Mungu kumuona tena Ray C akiwa mzima pamoja na ukimya wake katika muziki.
Ray C amekuwa akitundika picha hizo kwa ajili ya mashabiki na marafiki hasa kupitia Instagram akiambatanisha na maelezo huku nyingine zikizungumza zenyewe.

HATAKI KUTAJA ANAPOISHI
Maelezo ya picha hizo yamekuwa yakielezea maisha ya Ray C kwa sasa akiwa kwenye mjengo wa maana bila kutaja ni sehemu gani.
Kwa mujibu wa mashabiki wa Ray C, mwanadada huyo kwa sasa anakula bata tu huku akimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete ambaye anamuita ‘Daddy’ kwa kuwa ndiye aliyemsaidia kimatibabu.

DAKTARI ANASEMAJE?
Daktari mmoja maarufu jijini Dar aliyehojiwa na gazeti hili, alibainisha kuwa kinachosemwa na mashabiki wa Ray C kwamba kinachomnenepesha ni dozi ya kuacha madawa ya kulevya, kinaweza kuwa kweli au kisiwe kweli.
Aliongeza kuwa kunenepa kunachangiwa na vitu vingi kama kupata maisha mazuri yasiyohusisha msongo wa mawazo au mihangaiko ya hapa na pale hivyo anachofanya ni kula, kulala na kustarehe tu.

0 comments: